Monday, October 17, 2011

Waziri Mkuu - Mizengo Pinda
WAZIRI MKUU Mizengo Pinda amesema wakati Serikali inapiga mbiu ya uwekezaji, itahakikisha kuwa uwezekezaji mkubwa unaofanyika katika kilimo unawanufaisha wakulima wadogo ambao wanazunguka maeneo watakayopewa wawekezaji.
Ametoa kauli hiyo leo jioni (Jumapili, Oktoba 16, 2011), wakati akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kukagua mabanda ya maonesho nje ya ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mpanda ambako mkutano mkubwa wa uwekezaji wa Kanda ya Uwekezaji ya Ziwa Tanganyika (Lake Tanganyika Investors’ Forum) utafanyika.
Mkutano huo ambao utafunguliwa na Rais Jakaya Kikwete kesho asubuhi (Jumatatu, Oktoba 17, 2011), unalenga kuinua Kanda ya Uwekezaji ya Ziwa Tanganyika ambayo inaihusisha mikoa ya Rukwa, Kigoma na mkoa mpya-tarajiwa wa Katavi ambayo yote kwa pamoja imejaaliwa maliasili nyingi zikiwemo madini, vivutio vya utalii, ardhi nzuri ya kilimo na maeneo ya uvuvi.
Kuhusu maonesho hayo, Waziri Mkuu alisema amevutiwa na banda la Mkoa wa Kigoma kwa sababu wamejipanga vizuri chini ya mpango wao wa miaka 10 wa Kigoma Special Ecomonic Zone (KiSEZ 2009 – 2019) kwa kutenga hekta 20,000 zitakuwa na maeneo ya kilimo, viwanda na uendelezaji miji. Awamu ya kwanza ya KiSEZ yenye hekta 700 imeshapimwa na miundombinu inaandaliwa kuboreshwa katika eneo hilo.
Vilevile, alisema amefurahishwa na banda la Halmashauri ya Mpanda ambako ameelezwa kuwa wameunda kamati ya uwezekezaji yenye watu wanane chini ya mwenyekiti wao na kwamba mtu yeyote mwenye shida ya kuwekeza katika eneo lolote lile ni lazima apitie katika kamati hiyo.
“Ile kamati ni kama TIC vile (Kituo cha Uwekezaji), mtu anasema ni eneo gani la uwekezaji anataka na wao wanaangalia kama fursa hiyo ipo na kumpitisha katika taratibu zote… mfumo huu ni mzuri kwa sababu utaepusha mianya ya watu wajanja wachache kujinufaisha,” alisema.
Alisema nia ya mfumo huo ni kuweka kiungo kati ya wawekezaji na wananchi na pia kulinda ubia uliopo baina yao. “Tunataka wananchi wapate manufaa na huyo mwekezaji kama vile kupata zana bora za kilimo, mbegu bora, kupata masoko,” alisisitiza.
“Tunachokitaka hapa ni kuona teknolojia zao na uwepo wao unawasaidiaje wakulima wadogo… tufanye kilimo lakini na usindikaji pia. Wananchi wapate masoko lakini na bei ziwe za kuwanufaisha wakuliwa wetu,” alifafanua.
Waziri Mkuu Pinda ambaye aliwasili jana jioni (Jumamosi, Oktoba 15, 2011) kutoka Brazil na Marekani alikokuwa kwa ziara ya kikazi, amewasili Mpanda mkoani Rukwa leo mchana (Jumapili, Oktoba 16, 2011) na kukagua ukumbi wa mkutano ikiwa ni pamoja na mabanda ya maonesho yenye kueleza fursa za uwekezaji katika mikoa hiyo.

No comments:

Post a Comment