Friday, December 2, 2011

KWAHERI MR. EBBO

Msanii Mr Ebbo afariki dunia leo akiwa mkoani Arusha ambapo inasemekana alikuwa akiumwa katika hospitali ya Mount meru.Mr Ebbo alishawahi kufanya vizuri na wimbo wake wa "mi mmasai"

Thursday, November 24, 2011

STAR TIMES YAPATA KIBALI CHA KURUSHA MATANGAZO YA TELEVISHENI ZANZIBAR

Makamu wa kwanza wa Rais wa Zanzibar maalim Seif Sharif Hamad akipokea zawadi ya kompyuta ya dijital kutoka kwa Naibu Waziri wa mawasiliano ya Habari wa China Li Wei katika shamrashamra za uzinduzi wa kampuni ya Star Times ya China ambayo imepewa leseni kuendesha shughuli zake za matangazo ya Televisheni kwa dijital hapa Zanzibar.
Maalim Seif akizungumza katika uzinduzi wa kampuni ya Star Times ya China huko Hoteli ya Zanzibar Beach Resort Zanzibar.
Maalim Seif akipongezana na Naibu Waziri wa habari wa China baada ya uzinduzi wa kampuni ya Star Times. Kulia ni Waziri wa habari, utamaduni, Utalii na Michezo Zanzibar Abdillahi Jihadi Hassan. (Picha, Salmin Said- OMKR).

Hassan Hamad (OMKR)

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imetoa kibali rasmi cha kuiruhusu kampuni ya Star Times ya China kuendesha shughuli zake za matangazo ya televisheni kwa kutumia mfumo wa kisasa wa dijital.

Akizindua mpango huo huko hoteli ya Zanzibar Beach Resort Zanzibar, Makamu wa kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad amesema kuwepo kwa kampuni hiyo kutakuza ushirikiano wa muda mrefu kati ya China na Zanzibar.

Ameitaka kampuni hiyo kuendesha shughuli zake kwa kuzingatia maadili ya wazanzibari sambamba na kufuata sheria za nchi, na kwamba serikali itafanya kazi bega kwa began a kampuni hiyo katika kuhakikisha kuwa inaendesha shughuli zake bila usumbufu.

Amesema licha ya kampuni hiyo kuwepo kibiashara, lakini itasaidia kutoa ujuzi kwa wazalendo, pamoja na kutoa nafasi za ajira kwa vijana wa Zanzibar ambao wengi wao wanasomea sekta ya habari bila ya uhakika wa ajira zao.

Amefahamisha kuwa China ni rafiki wa kweli wa Zanzibar na kwamba serikali inathamini sana mchango wa nchi hiyo katika nyanja mbali mbali za maendeleo na bado inakaribisha makampuni zaidi ya kichina kuja kuwekeza miradi yao.

Ameiomba kampuni hiyo pia kuzingatia hali ya uchumi wa Zanzibar, ili waweke viwango vya malipo ambavyo wazanzibari wengi wataweza kuvimudu na kuitumia televisheni hiyo kwa kupata taaluma na burudani zitakazotolewa.

Kampuni ya Star Times ya China ni kampuni ya mwanzo ya kigeni kuruhusiwa kuendesha shughuli hizo za habari hapa nchini, lakini tayari inaendesha shughuli zake kwa mikoa saba ya Tanzania Bara na ina wateja wapatao 140,000.

Mwenyekiti wa kampuni hiyo Pang Xin Xing amesema leseni hiyo ni hatua muhimu katika kufikia matarajio yao ya kukuza ushirikiano na kuelimisha jamii juu ya mambo mbali mbali ya maendeleo, tamaduni na kukuza biashara.

Kabla ya uzinduzi huo Makamu wa kwanza wa Rais alikutana na Naibu Waziri wa mawasiliano ya habari wa China Bw. Li Wei ambaye ameelezea matumaini yake ya kuendelea kwa uhusiano wa muda mrefu baina ya pande hizo mbili.

Bw. Li amesema ushirikiano uliopo haulengi baina ya serikali kwa serikali pekee bali unatapakaa katika nyanja mbali mbali zikiwemo vyombo vya habari wakati ambapo tayari matangazo ya Televisheni ya taifa ya China ya CCTV News na yale ya Radio China Kimataifa CRI yanapokelewa vizuri na wananchi wa Zanzibar.

KUKIMBILIA SEKTA BINAFSI KWA WATAALAM NI ATHARI KUBWA KWA SEKTA YA UMMA


Na Nafisa Madai Maelezo -Zanzibar

WAZIRI wa Sheria na Katiba, Abubakari Khamis Bakary, amesema kasi ya wataalamu wanaokimbilia sekta binafsi, imekuwa na athari kubwa katika kuleta ufanisi na mageuzi katika sekta ya umma.

Hayo aliyaeleza wakati akifungua warsha ya maendeleo ya rasilimali watu kwa wataalamu wa Shirikisho la Mawasiliano la Kusini mwa Afrika (SATA), kwaniaba ya Waziri wa Miundombinu na Mawasiliano na Uchukuzi huko katika ukumbi wa hoteli ya Zanzibar Ocean View mjini zanzibar.

Waziri huyo alisema baadhi ya watu wanaona utaratibu huo ni njia muafaka kwa kuwa watalaamu wanapata fursa ya kuchangia ujuzi wao katika sekta zote za uchumi.

Waziri Bakary, alisema mtazamo huo unahitaji kuungwa mkono na wote kwa kuwa sekta binafsi na umma zina nafasi sawa katika ujenzi wa uchumi katika mataifa hayo.

Alisema Zanzibar kama sehemu ya dunia imekuwa ikipoteza wataalamu wake wengi, wanaokwenda kufanya kazi katika nchi nyengine, wakitafuta uzoefu na maslahi zaidi.

Waziri Bakary alisema hakuna nchi yoyote duniani inayoweza kuwadhibiti au kuwafungia wataalamu wake wasitoke ndani ya nchi zao, lakini kama nchi wanachohitaji kukifanya ni kutengeneza fursa za ajira pamoja na kulipa mishahara mizuri kwa ajili ya wataalamu wa ndani.

Naye Mtendaji Mkuu wa Posta Tanzania, Said Amir.Said alisema, teknolojia ya mawasiliano imekuwa ikibadilika haraka sana hivyo lazima wataalamu wa mawasiliano nao kubadilika kwa ajili ya rasilimali watu.

Aidha alieleza mkutano huo umekuwa fursa nzuri kwa Zanzibar kutambulika wakati huu mkonga wa mawasiliano ukitarajia kuchukua nafasi katika visiwani vya zanzibar

Jumla ya wataalamu wa nchi 10 za Shirikisho la SATA walishiriki katika mkutano huo zikiwemo Msumbiji, Botswana, Namibia, Zimbabwe, Afrika Kusini, Malawi, Zambia na Tanzania.

Mkutano huo wa siku tatu ambao unatarajiwa kufungwa leo hii wataalamu hao wataweza kupata fursa ya kutembelea maeneo kadhaa ya mji wa zanzibar ikiwemo kizimbani ambako watakagua mashamba ya spice, mji mkongwe.

MASHIRIKIANO ZAIDI YANAHITAJIKA KUTOKOMEZA MIFUKO YA PLASTIKI: MAALIM SEIF

Kamishna wa polisi Zanzibar Mussa Ali Mussa akitoa rai mbele ya makamu wa kwanza wa Rais maalim Seif Sharif hamad katika kufanikisha operesheni za kutokomeza mifuko ya Plastiki Zanzibar.
Maalim Seif akizungumza na kikosi kazi cha kupambana na mifuko ya plastiki ukumbi wa mikutano katika OMKR Migombani.(Picha, Salmin Said- OMKR)

Hassan Hamad (OMKR).

Makamu wa kwanza wa Rais wa Zanzibar maalim Seif Sharif Hamad amesema mashirikiano zaidi yanahitajika katika kutokomeza matumizi ya mifuko ya plastiki Visiwa Zanzibar.

Sambamba na hilo Maalim Seif amesisitiza elimu zaidi itolewe kwa wananchi ili kutambua athari za matumizi ya mifuko hiyo ambayo imekuwa ikilalamikiwa kuwa chanzo kikuu cha uchafu katika manispaa ya mji wa Zanzibar.

Maalim Seif alikuwa akizungumza na kikosi kazi cha kupambana na matumizi ya mifuko ya plastiki huo Ofisni kwake migombani, kinachowashirikisha watendaji 10 wakiwemo kutoka jeshi la polisi, Wizara ya Biashara na idara ya Mazingira.

Amesema licha ya mafanikio yaliyopatikana tangu kikosi kicho kizinduliwe rasmi na kuanza kazi miezi michache iliyopita, bado juhudi zaidi zinafaa zichukuliwe kwa kulishirikisha kikamilifu jeshi la polisi katika operesheni zinazofanywa za kuisaka mifuko ya plastiki na kuifanya Idara ya mazingira kuwa mratibu mwezeshaji wa operesheni hizo.

Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa kwanza wa Rais Mhe. Fatma Abdulhabib Fereji ambaye alishiriki katika mazungumzo hayo amesema ni vyema kikosi hicho kikaangaliwa upya ili kutoa fursa kwa jeshi la polisi kuongoza operesheni hizo.

Mhe. Fereji pia ameahidi kusimamia kanuni za sheria ya kutoa adhabu kwa watu watakaopatikana na mifuko hiyo ambayo kwa ujumla inakaribia kukamilika na kuchapishwa katika gazeti rasmi la serikali ili iweze kufanya kazi.

Kikao hicho pia kilihudhuriwa na kamishna wa polisi Zanzibar Mussa Ali Mussa amesema bado kuna fursa nzuri ya kufanikiwa kwa operesheni hizo iwapo zitawahusisha viongozi wa shehia na kutekeleza mpango wa polisi jamii katika visiwa vya Unguja na Pemba.

Watendaji wa kikosi hicho kwa upande wao wameelezea changamoto zinazowakabili ikiwa ni pamoja na ukosefu wa vitendea kazi hasa usafiri, pamoja na kutokuwepo sheria madhubuti ya kuwahukumu wanaokamatwa na mifuko hiyo.

Wamesema hali hiyo inawafanya wananchi kutokuwa na hofu kwa vile hakuna sheria inayowabana, na hivyo kulifanya zoezi hilo kuwa gumu.

Kikosi kazi hicho kimeiomba serikali kusimamia utekelezaji wa maagizo yake katika mamlaka zinazohusika, wakidai kuwa mifuko mingi kati ya inayoingia nchini inapitia katika bandari kuu ya Zanzibar huku watendaji wa mamlaka hiyo wakifumbia macho agizo hilo.

CHAMA CHA DEMOKRASIA NA MAENDELEO (CHADEMA) KURUGENZI YA HABARI NA UENEZI –MAKAO MAKUU TAMKO KWA UMMA WA WATANZANIA


YAH: KAMATI KUU YA CCM KUMWAGIZA RAIS KIKWETE AKUTANE NA VYAMA VINGINE VYA SIASA

Kurugenzi ya Habari na Uenezi imeshangazwa na tamko lililotolewa jana na Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM ndugu Nape Nnauye kuwa “Kamati Kuu ya CCM imemwagiza Mwenyekiti wa Chama hicho, Rais Jakaya Kikwete akutane na vyama vyote vya siasa badala ya CHADEMA peke yake” aliendelea Kusema kuwa …… “Pamoja na kukubali akutane na CHADEMA, tumetahadharisha kuwa lazima kushirikisha wajumbe wengine kutoka kwenye vyama vyenye uwakilishi ndani ya Bunge isiwe CHADEMA pekee”.


Awali ya yote tunapenda kusisitiza kuwa maridhiano ya kitaifa juu ya mchakato wa kuweza kufikia kupata katiba mpya ni suala ambalo ni la muhimu sana kwa mustakabali wa taifa letu na haswa kama muafaka huo utafikiwa kwa nia njema ya kujenga na kuimarisha mshikamano miongoni mwa watanzania bila kujali dini, rangi, kabila ama itikadi za vyama vyao.


Tamko la Kamati Kuu ya CCM linaonyesha muendelezo wa matamko ambayo wamekuwa wakiyatoa kila mara wanapokutana, mathalani kikao kilichopita kiliiagiza serikali kuwa bei ya mafuta ya taa lazima ishuke, kitu ambacho mpaka leo hakijafanyiwa kazi na hii inaonyesha jinsi ambavyo Kamati kuu hiyo isivyokuwa na msimamo juu ya maamuzi yake na maagizo yake inayotoa kwa viongozi wa kiserikali.


Tamko hili, limetushangaza kwani limeonyesha wazi kuwa kuna hofu miongoni mwa viongozi na wajumbe wa Kamati Kuu ya CCM kuwa sheria iliyopitishwa na wabunge wa CCM kwa kushirikiana na wale wa CUF haina muafaka wa kitaifa na hivyo wanamwagiza Rais kukutana na makundi mengine ili kupata maoni kabla ya kuisaini sheria hiyo.


CHADEMA tuliandika barua kwa Rais naye alikubali kukutana nasi, kitendo cha Kamati Kuu ya CCM kutoa tamko hili ni dhahiri kuwa kamati kuu ya CCM imejitwalia madaraka ya kuwa wasemaji wa vyama vingine vyenye uwakilishi Bungeni ambao mpaka leo hatujawasikia wakitoa tamko juu ya suala hilo. Tunajiuliza hivi Kamati Kuu ya CCM leo imekuwa ndio wasemaji wa vyama vyenye uwakilishi Bungeni ukiiondoa CHADEMA?


Pili, Vyama vyenye uwakilishi Bungeni ukiiondoa CHADEMA NA NCCR-Mageuzi waliopinga muswada huu, vyama vingine mathalani CUF, CCM na TLP wao waliunga mkono kupitishwa kwa muswada huu, sasa Kamati Kuu ya CCM inataka wakakutane na Rais ili kujadili kitu gani? Wakati walikuwa ni sehemu ya maamuzi ambayo CHADEMA na wadau mbalimbali wanayalalamikia na ndio maana tukataka kuwasilisha malalamiko yetu kwa Rais.


Tunapenda kuikumbusha Kamati Kuu ya CCM kuwa CHADEMA iliomba kukutana na Rais wa Nchi na sio kama Mwenyekiti wa chama, iwapo Rais atakubaliana na agizo hili la Kamati Kuu ya CCM itakuwa dhahiri kuwa ni muendelezo wa ushahidi kuwa viongozi wa Kiserikali wamekuwa wakitimiza majukumu yao kutokana na shinikizo la Chama hata kwenye masuala ambayo ni muhimu kwa mustakabali wa taifa letu kama suala hili la Katiba lilivyo.


Mwisho, Tungependa kumshauri Rais kuwa pamoja na kukutana na CHADEMA atenge muda ili aweze kukutana na makundi mengine mbalimbali ya kijamii yenye maoni na malalamiko kabla ya kusaini sheria iliyopitishwa na Bunge kwa maslahi ya taifa letu na ili kuweza kuleta utengamano wa kitaifa .Imetolewa na:

Erasto TumboMkurugenzi wa Habari na Uenezi24 Novemba 2011.

SMZ YAKUSUDIA KUKIENDELEZA CHUO KIKUU SUZA KIWE MFANO AFRIKA MASHARIKI NA AFRIKA NZIMA

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Cha Taifa cha Zanzibar SUZA Profesa Idrisa Rai akimueleza Makamu wa kwanza wa Rais Maalim Seif Sharif Hamad malengo ya chuo hicho huko OMKR migombani.

Hassan Hamad (OMKR).

Serikali ya mapinduzi ya Zanzibar imesema inakusudia kukiendeleza Chuo Kikuu Cha Taifa SUZA ili kiwe mfano katika ukanda wa Afrika Mashariki na Bara zima la Afrika.

Kauli hiyo imetolewa na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad ofisini kwake migombani alipokutana na Makamu Mkuu wa Chuo hicho Profesa Idrisa Rai.

Amesema inawezekana kwa chuo hicho kupata mafanikio makubwa kutokana na mipango yake imara ya kuimarisha miundombinu ya majengo pamoja na kuanzisha vitivo mbali mbali vya masomo yanayokwenda na wakati.

Ameuomba uongozi wa chuo hicho kufikiria pia kuanzisha kituo cha utafiti wa kilimo hasa kwa zao la karafuu ikizingatiwa kuwa hilo ni zao tegemeo katika uchumi wa Zanzibar.

Aidha ameunga mkono malengo ya chuo hicho kuweka msisitizo katika taaluma ya habari na mawasiliano ICT kwani ina mchango mkubwa katika maendeleo ya sasa ya sayansi na teknolojia.

Kwa upande wake Makamu Mkuu wa Chuo hicho Profesa Idrisa Rai amesema Chuo hicho kinakusudia kupanua huduma zake kwa kuingiza taaluma mbali mbali ambazo zitasaidia maendeleo ya jamii.

Amezitaja baadhi ya taaluma hizo kuwa ni pamoja na utalii, kilimo, habari na mawasiliano, sambamba na kutoa mafunzo ya ngazi ya shahada ya pili na tatu kwa fani ya Kiswahili.

Amesema Chuo kimezingatia umuhimu wa kuliendeleza somo la Kiswahili ikizingatiwa kuwa Zanzibar ndio kitovu cha lugha hiyo ambayo mahitaji yake yamekuwa yakiongezeka siku hadi dunia.

Amesema wanakusudia kuitangaza lugha hiyo ili kila mgeni atakayehitaji kujifunzi lugha hiyo afike Zanzibar badala ya kwenda nchi nyengine na kwamba mafanikio ya Kiswahili yataitangaza Zanzibar kiutalii duniani kote.

Aidha Profesa Rai amesema chuo hicho pia kina malengo ya kuwaendeleza wakufunzi wake kwa kuwapa elimu ya kiwango cha juu ili waweze kuisambaza elimu hiyo kwa wanafunzi, na kukifanya chuo hicho kiwe na sifa ya kujivunia ya kutoa elimu bora ambayo pia itanyanyua kiwango cha elimu Zanzibar.

Wednesday, November 23, 2011

WATANZANIA WAISHIO UJERUMANI WAANZA SHAMRA SHAMRA ZA KUSHEREHEKEA MIAKA 50 YA UHURU WA TANZANIA BARA


Watanzania wanaoishi Ujerumani ! na Full Shangwe ya Miaka 50 ya Uhuru !
Kuanzia München hadi Berlin Chereko !Chereko !

FFU wa Ngoma Africa Band kutoa burudani ya kukata na Mundu !

Umoja wa Tanzania Ujerumani (UTU) kuzinduliwa rasmi ! 10-12-2011 Berlin!


Watanzania waishio Ujerumani wameanza shamra shamra za kusherekea miaka 50 ya uhuru
wa Tanzania bara, kwa kasi kubwa inayotingisha kila kona,sherehe hizo zinaanzia mjini
München siku ya 3 Dec 2011 ambapo kutakuwa na maonyesho mbali mbali ya bidhaa za
Tanzania,mavazi,na mdahalo rasmi na usiku kutakuwa na muziki wa Ngoma Africa Band
katika mtaa wa Siebold Str,11 ndipo penye ukumbi.

Kuanzia 9 hadi 10-Dec-2011 mjini Berlin ambako ndipo hupo Ubalozi wa Tanzania na ndio
mji mkuu wa Ujerumani,kutakuwa hapatoshi kwani sherehe hizo zitaambatana na ufunguzi
wa UMOJA WA WATANZANIA UJERUMANI (UTU) 

Siku ya jumamosi 10-12-2011, umoja huo unawaunganisha watanzania wote waishio ujerumani,ulitiliwa nguvu na balozi Mh.Ngemera, umeshasajiliwa na viongozi wake ni Bw.Mfundo Peter Mfundo(mwenyekiti) na Bi.Tullalumba Mloge (katibu),utaratibu unaonyesha kuwa sherehe hizo mjini Berlin zitaanza saa 9 mchana hadi usiku usio kwisha ambapo Ngoma Africa Band aka FFU,watatumbuiza na muziki wao,mahala patakapo fanyika sherehe Apostelkirche 1, 10738 Berlin,

UMOJA NI NGUVU WATANZANIA JITOKEZENI ! KUSHREKEA MIAKA 50 YA UHURU !
sikiliza muziki at www.ngoma-africa.com

TIMU YA TAIFA YA ZANZIBAY YAAGWA NA KUKABIDHIWA BENDERA YA TAIFA TAYARI KWA CHALLENGE

Waziri wa habari utamaduni utalii na michezo Abdilah Jihad Hassan akimkabidhi bendera nahodha wa timu ya Taifa ya Zanzibar Agrey Moris huko kikwajuni mjini zanzibar katika sherehe za kuwaaga wachezaji wa timu hiyo wanaokwenda kweye michuano ya Tusker Cecafa Challenge Cup 2011
Waziri wa Habari Utamaduni utalii na michezo akizungumza na wachezaji wa timu ya taifa ya Zanzibar katika hafla ndogo ya kuwaaga iliyofanyika kikwajuni mjini zanzibar kushoto ni naibu waziri wa habari utamaduni utalii na michezo Bihindi Hamad Khamis na kulia ni Rais wa chama cha soka cha zanzibar Ali Fereji tamimu
Wachezaji wa timu ya Taifa ya Zanzibar, Zanzibar heroes wakiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa Wizara ya habari pamoja na viongozi wa chama cha soka cha Zanzibar

Na Hamad Hija Maelezo Zanzibar

Waziri wa Habari Utamaduni Utalii na Michezo Jihad Abdilah Hassan amsema kuwa timu ya taifa ya Zanzibar ni timu yenye uwezo mkubwa na anaamini kuwa timu hiyo itafanya vizuri katika michuano ya kombe la challenge itakayoanza wiki hii huko jijini Darsalaam

Waziri Jihad ameyasema hayo leo huko katika ukumbi wa Wizara ya habari ulioko Mnazi Mmoja Mjini Zanzibar wakati akiiaga na kuikabidhi bendera timu ya Taifa Zanzibar, Zanzibar Heroes inayokwenda kushiriki michuano ya challenge.

Waziri huyo wa habari amefafanuwa zaidi na kusema kuwa lengo la kushiriki mashindano kwa timu hiyo, ni kuleta ushindi na kwa kuwa timu imeandaliwa vizuri ikilinganishwa na miaka ya nyuma, inasababu kubwa ya kufanya vizuri.

Waziri amesema, hivi sasa timu ya Zanzibar Heroes inatisha kutokana na maandalizi makubwa yaliyofanywa na timu hiyo,ikiwemo kuweka kambi ya wiki mbili Nchini Misri hatua ambayo ni sababu ya msingi kwa timu hiyo kuipeperusha vyema b endera ambayo wamekabidhiwa.

AidhaWaziri Jihad amesema kuwa mashindano ni mashindano hivyo timu iwemakini katika kucheza mpira na ifuate sheria kumi na saba za mchezo ndicho kitu pekee ambacho kitawasaidia wakati wa michezo na wakati mashindano yanapoendelea nchini humo.

Aidha Waziri amesema kuwa mashindano ni sawa na vita hivyo timu ya Taifa ya Zanzibar inatakiwa ipigane kufa na kupona ili iweze kufanya vizuri katika michuano hiyo ya challengeambayo yanafanyika jijini Darsalamm ikiwa inazishirikisha timu za ukanda huu wa Afika Mashiriki ambapo timu ya Somalia Uganda Kenya Tanzania ni miongoni mwa timu zinazotegemewa kushiriki katika mashindano hayo

Na kwa upande wa kocha wa timu hiyo ya Taifa ya Zanzibar (Zanzibar heroes) Hemed Suleiman Moroko amesema kuwa, kwa mara ya pili wanategemea kulileta kombe hilo hapa Zanzibar kwa vile timu hiyo imepata maandalizi ya kutosha

Amesema kuwa kwa mara ya kwanza timu ya Taifa ya Zanzibar ilileta kombe mwaka 1995 kutoka Nchini Uganda na mwaka huu wa 2011 timu hiyo na kukusudia kuleta tena kombe hilo kutoka Tanzania bara.

Naye Kapteni wa timu hiyo ya Taifa ya Zanzibar Agrey Moris, amewaahidi wananchi wa zanzibar kwamba wataipeperusha vyema bendera ya Zanzibar,kutokana na kuwa wamejipanga vizuri katika michuano hiyo ya kombe la challenge linalotegewa kutimua vumbi mwishoni mwa wiki hii


Wakati huo benki ya watu wa Zanzibar PBZ imetowa jumla ya shilingi millioni mbili ikiwa ni mchango wao kwenye timu hiyo ya Taifa fedha hizo zimekabidhiwa leo katika hafla hiyo ya kuagwa kwa timu ya Taifa na Meneja Masoko wa benki hiyo ya Zanzibar Juma Amuor ame

CHANGAMOTO KUBWA INAYOLIKABILI BARA LA AFRIKA

Changa moto kubwa inayolikabili Bara la Afrika Hivi sasa katika kuelekea kwenye Maendeleo zaidi ni kutumia mbinu na Marifa yaliyopelekea kupunguza migogoro ya Jamii na baadhi ya Mataifa ndani ya Bara hili.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi ametoa kauli hiyo wakati akifungua Mkutano wa Tatu wa Viongozi na Wataalamu wanaoshughulikia Kuondosha migogoro Barani Afrika unaofanyika huko katika Hoteli ya Melia iliyopo Pwani Mchangani Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Balozi Seif alisema Jamii ya Kimataifa imeshuhudia utatuzi wa Migogoro kadhaa Barani Afrika hali ambayo kwa kiasi kikubwa imepunguza Migogoro na hata Mauaji ya Raia wasio na hatia.

Aliwataka Viongozi na Wataalamu hao kutumia fursa nzuri iliyopo ya Amani iliyorejea Barani humu kwa kuweka Mipango bora itakayoleta faraja zaidi ya ustawi wa Jamii katika miaka ijayo.

“ Tumeshuhudia utulivu wa Kisiasa ilivyorejea ndani ya Bara hili hasa katika Ukanda wa Maziwa Makuu eneo ambalo Sudan na Jmuhuri ya Kidemokrasi ya Congo { DRC } zilikuwa katika migogoro mikubwa ya Kisiasa ”. Alikumbusha Balozi Seif.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alielezea matumaini yake kwamba Ripoti itakayotolewa na Viongozi hao baada ya kumalizika Mkutano wao itawezesha kujenga mazingira bora ya kudumisha Amani Barani Afrika.

Balozi Seif amezipongeza Taasisi zilizoandaa Mkutano huo ile ya Mwalimu Nyerere, Kituo cha Hali za Binaadamu cha Kimataifa na Wizara ya Mambo ya Nje ya Norway kwa uamuzi wao wa kufanya Mkutano huo Hapa Zanzibar na hasa ndani ya Jimbo lake ya Kitope.

Alisema uwamuzi wao huo haukuwa wa kubahatisha bali imekuja kwa kuzingatia sifa ya Zanzibar ya amani iliyopelekea kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa { GNU } kufuatia Mgogoro wa muda mrefu uliovihusisha Vyama vya CCM na CUF.

Balozi Seif aliwaeleza Washiriki wa Mkutano huo kwamba Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar inafanya kazi zake vyema huku ikikabiliwa na changa moto kubwa ya kutekeleza matarajio ya Wananchi wote wa Zanzibar.

Akimkaribisha Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere Dr. Salim Ahmed Salim alisema yapo Maendeleo makubwa ya kupunguka kwa Migogoro Barani Afrika jambo ambalo limeleta faraja kwao akiitolea mfano nchi ya Sudan.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Kituo cha Kimataifa cha Haki za Binaadamu bwana David Harland ameipongeza Zanzibar kwa ukarimu wake unaopelekea kupokea Vikao na Mikutano Mzizito ya Kimataifa ndani na nje ya Bara la Afrika.

Wakati wa Mchana akiwa Mkoani Dodoma Makamu wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alikutana wa Uongozi wa Kampuni ya uwekezaji vitega uchumi inayojishughulisha na Mradi wa umeme unaotumia upepo na jua kutoka Nchini India.

Mkurugenzi mkuu wa Kampuni hiyo ya Indomount bwana sudhakar amesema Taasisi yake imepanga kutumia Jumla ya Dola za Kimarekani Bilioni Moja kati ya Bilioni saba zilizotengwa na waziri mkuu wa Nchi hiyo kusaidia Serikali na Taasisi Binafsi Barani Afrika.

Naye Balozi Seif ameuomba Uongozi wa Kampuni hiyo kuangali Meneo ambalo wanaweza kusaidia kati ya yale yaliyoainishwa na kupendekezwa na Zanzibar katika mipango yake ya Maendeleo.



Othman Khamis Ame

Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

23/11/2011.

Tuesday, November 22, 2011

WAZANZIBARI KWA NAFASI ZAO WATAKIWA KUTUMIA FULSA MUHIMU ILIYOPO KUJADILI MSWADA WA SHERIA

Faki Mjaka na Zahira Bilal-Maelezo, Zanzibar

Waziri wa Katiba na Sheria Zanzibar Abubar Khamis Bakar amewasihi Wazanzibari kwa nafasi zao watumie fursa muhimu iliyopo kwa sasa kujadili Mswada wa Sheria ya Katiba kwa lengo la kupata Katiba Mpya yenye maslahi ya Wazanzibari na Watanzania kwa ujumla. 

Waziri huyo ameyasema hayo leo katika Ukumbi wa Baraza la Wawakilishi la zamani Kikwajuni Zanzibar alipokuwa akizungumza na Wananchi,Wanasiasa pamoja na Waandishi wa Habari kuhusiana na Mswaada wa Utaratibu wa kupatikana kwa Katiba Mpya.

Amesema upatikanaji wa Katiba Mpya yenye maslahi kwa Wazanzibari inatokana na kuwepo kwa umoja na uzalendo ambao unatanguliza maslahi ya Zanzibar mbele na siyo kujali maslahi ya Vyama.

Abuubakar amewataka pia wananchi wa Zanzibar kujikusanya na kuipitia Katiba iliyopo na kuyajadili mapungufu yaliyomo katika katiba hiyo ili muda utakapofika wa kutoa maoni juu ya Katiba Mpya waweze kufanya hivyo.

Aidha amesema mswaada huo Mpya ambao umepitishwa karibuni na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambao pia unasubiri kutiwa saini na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni mzuri na wenye kujali maslahi ya Zanzibar.

Waziri huyo wa Katiba na Sheria Zanzibar amewatahadharisha wananchi kuwa makini na watu ambao wanaweza kuwapotosha wananchi katika kipindi hiki cha kujadili mchakato wa kupata Katiba Mpya.

Amesema kwamba wananchi wanapaswa kuitumia fursa adhimu waliyoipata kipindi hiki na kwamba kama hawatoitumia vizuri wanaweza kuijutia katika maisha yao.

Kwa upande wa wananchi waliochangia katika mkutano huo wamewaomba viongozi na wanasiasa kupita katika Majimbo yao ili kuendelea kuwaelimisha wananchi juu ya upatikanaji wa Katiba Mpya

Aidha wameviomba vyombo vya Habari Zanzibar kuandaa vipindi mbalimbali na kushiriki kikamilifu katika Makongamano na Warsha mbali mbali juu ya Upatikanaji wa Katiba hiyo

Mkutano huo ambao ulikuwa wa aina yake na kuhudhuriwa pia na baadhi ya Mawaziri wa Seririkali ya Mapinduzi ya Zanzibar wananchi walipata fursa ya kutoa maoni yao juu ya Mswaada huo.

KONGAMANO LA MSWAADA JUU YA KUKUSANYA MAONI YA KATIBA MPYA, WADAU WATAKA MUUNGANO UVUNJWE!

WANANCHI WA ZANZIBAR WAMEPATA MWAMKO MZURI KATIKA VITA DHIDI YA MAAMBUKIZI MAPYA YA VIRUSI VYA UKIMWI: SMZ

Waziri wa nchi, Ofisi ya Makamu wa kwanza wa Rais anayehusika na mambo ya UKIMWI Mhe. Fatma Abdulhabib Fereji akiwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Ukimwi Zanzibar ZAC Dr. Omar Makame Shauri katika mazungumzo na Waandishi wa ahabri juu ya maadhimisho ya siku ya Ukimwi Duniani yanayofikia kilele chake Disemba 01, 2011.
Mhe. Fatma Ferej akizungumza na waandhishi wa habari juu ya maadhimisho.
Mhe. Fatma Ferej akizungumza na waandhishi wa habari juu ya maadhimisho.
Waandishi wa habari wa vyombo mbali mbali nchini wakisikiliza hotuba ya Mhe. Fatma Ferej kuhusiana na maadhimisho ya ya siku ya Ukimwi duniani. Hafla hiyo ilifanyika OMKR Migombani Zanzibar. (Picha, Salmin Said, OMKR).

Na: Hassan Hamad. (OMKR)

Serikali ya Mapinduzi ya  Zanzibar  imesema wananchi wa Zanzibar wamepata  mwamko mzuri katika vita dhidi ya maambukizi mapya ya virusi vya UKIMWI na Unyanyapa dhidi ya watu wanaoishi na virusi vya ugonjwa huo.
Akizindua wiki ya kampeni ya maadhimisho ya siku wa UKIMWI duniani itakayofikia kilele chake tarehe 01 Disemba 2011 duniani kote, Waziri wa nchi, Ofisi ya Makamu wa kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Fatma Abdulhabib Ferej amesema mafanikio hayo yametokana ya juhudi kubwa zinazochukuliwa na Tume ya UKIMWI Zanzibar katika mapambano hayo.
Mhe. Fatma Fereji alikuwa akizungumza na waandishi wa habari wa vyombo mbali mbali ofisini kwake kufuatia maadhimisho hayo yatakayoadhimishwa kitaifa katika kijiji cha Makombeni, Wilaya ya Mkoani Pemba ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Rais wa Zanzibar Dkt. Ali Mohd Shein.
Amesema kwa sasa idadi ya maambukizi inabakia kuwa asilimia 0.6 kwa Zanzibar lakini kuna  makundi matatu ya vijana yameathirika zaidi. “Ukweli hali ya maambukizi kwa ujumla ni asilimia 0.6, lakini hali ni mbaya kwa watumiaji wa dawa za kulevya hasa wanaojidunga sindano ambao wameambukizwa kwa asilimia 16, kundi la wanawake wanaojiuza asilimia 10.8 na watu wanaofanya mapenzi ya jinsi moja asilimia 12”, alifafanua Mhe. Fereji.
Amefahamisha kuwa juhudi zaidi zinapaswa kuchuliwa ili kufikia wito wa kauli mbiu ya maadhimisho ya mwaka huu ambayo ni “Kuzifikia Sifuri tatu”, ikiwa na tafsiri ya kufikia asilimia zero ya maambukizi mapya, asilimia zero ya unyanyapaa na asilimia zero ya vifo vitokanavyo na UKIMWI ifikapo mwaka 2015.
Amesema kauli mbiu hiyo inaweza kufikiwa iwapo wadau wote wakiwemo wananchi watashirikiana katika kuondoa muhali wa kuwafichua watumiaji wa dawa za kulevya na kuhamasika kupima afya kila baada ya kipindi fulani.
“muhali ndio unaotuharibia wazanzibari, lakini ikiwa tutaondoa muhali kuwafichua watu hawa na kuepukana na unyanyapaa wa aina zote, bali malengo hayo ya sifuri tatu yatafikiwa”, alisema.
Amebainisha kuwa hali ya unyanyapaa imepungua kwa kiasi kikubwa ikilinganishwa na miaka iliyopita, hali inayopelekea baadhi ya wachumba kukubali kufunga ndoa, huku mmoja kati ya wapenzi hao akiwa ameathirika.
Ametoa wito kwa jamii ya kizanzibari kufuata maadili yao ambayo ndio kinga pekee ya maambukizi mapya, akitoa mfano kuwa makundi yote matatu yaliyoathirika zaidi yanafanya mambo hayo kinyume na maadili ya Wazanzibari na dini.
Mhe. Fereji amekwenda mbali zaidi pale akipotoa onyo la kumuwajibisha mtendaji yeyote wa Ofisi yake atakayebainika kuendeleza unyanyapaa dhidi ya watu wanaoishi ya VVU.
Akizungumza katika kikao hicho na waandishi wa habari, Mkurugenzi mtendaji wa Tume ya UKIMWI Zanzibar ZAC Dr. Omar Makame Shauri amesema kiasi ya shilingi milioni 30 zinatarajiwa kutumika kwa ajili ya maadhimisho hayo.
Amesema licha ya mafanikio yalioyopatikana, lakini bado kuna changamoto kwa baadhi ya wananchi kushindwa kubadili tabia na kuendeleza unyanyapaa, jambo ambalo tume yake inajaribu kutoa elimu kwa wananchi ili kutoa uelewa zaidi ya tatizo hilo.
Dr. Shauri ametoa wito kwa wananchi kuvitumia vituo vya ushauri nasaha na kupima VVU bila ya malipo, ili kutambua maendeleo ya afya zao kwa lengo la kuepusha maambulizi ya VVU na vifo vitokanavyo na janga hilo.

TAIFA CHANGA KAMA TANZANIA LINAKABILIWA NA CHANGAMOTO YA VIJANA AMBAO HAWAWEZI KUJITUMA NA KUJIAJIRI: HAJI USSI

Na Nafisa  Madai       Maelezo Zanzibar

Mkuu wa idara ya utawala na uwenezi katika chama cha mapinduzi mhe Haji Ussi Gavu amesema taifa changa kama Tanzania linakabiliwa na changamoto kubwa ya kutokua na vijana ambao wanaoweza kujituma na kujiari wenyewe.

Amesema taifa linakabiliwa na tatizo hilo linaweza kuzorota katika uwendeshaji wa shughuli zake za kila siku kwa kupoteza nguvu ngazi na rasilimali kazi ya vijana ambao wengi hivi wamekua wakijishulisha na kadhia za vigenge.

Gavu ambae pia ni naibu waziri wa miundombinu na mawasiliano ameyasema hayo alipokua akifunga mkutano mkuu wa baraza la vijana  katika wilaya ya Muheza mkaoni Tanga.

Aidha alisema taifa bila ya kuwepo kwa amani na utulivu linaweza kukosa amani hivyo aliwaasa vijana hao walinde amani na utulivu uliopo kwa sasa kwani uzoefu unaonesha vijana ndio vyanzo vya migogoro katika mataifa mbali mbali.

Hata hivyo alisema imani yake kubwa utulivu uliokuwepo unaletwa na CCM lakini kuna baadhi ya vyama kwa makusudi wanachochoe vijana katika vyuo  kufanya vurugu jambo ambalo limekua likitishia amani katika nchi hii.

“Matendo yanayoyafanywa na baadhi ya vyama vya siasa ni vya ajabu sana leo hii wanachochea vijana tena wanafunzi katika vyuo vikuu  hii dalili tosha  ya uharibifu wa amani katika chii yetu.””alisema Gavu.

Aidha aliwataka vijana hao waelekeze nguvu zao katika kilimo kama ilivyo azma ya serikali ya kutaka kuinua kilimo na kusema KILIMO KWANZA mbapo alisema iwapo watafanya hivyo changamoto  ya umaskini itawaondoka.

Aidha alisema  ili kujenga jeshi kubwa la kilimo lazima vijana wajitolee katika kilimo ili rasilimali iweze kubaki nchini na isichukulie

MCHUNGAJI ATEMBEZWA UCHI MTAANI ARUSHA

NA GLADNESS MUSHI WA FULLSHANGWE -ARUSHA 
 
MVUTANO mkubwa umeibuka baina ya jamii ya wafugaji (wanaoabudu mila na desturi) na wachungaji wa madhehebu mbalimbali ya kidini wilayani Arumeru na kusababisha baadhi ya wachungaji kuzikimbia familia zao wakihofia kuuawa. 
 
Katika hali isiyokuwa ya kawaida mchungaji wa kanisa la Matendo, (Pentekoste),Julius Lukumay (34)amekiona cha moto baada ya kujikuta akitembezwa uchi wa mnyama kwa siku mbili mfululizo na jamii hiyo ya wafugaji kwa madai ya kukataa kushiriki kikao cha kimila. Ilidaiwa ya kuwa adhabu hiyo imetokana na mchungaji Lukumay kukaidi kulipa faini ya shilingi 500,000 aliotozwa na jamii hiyo kwa kile kilichoelezwa kwamba aliwashitaki wazee wa kimila katika ofisi ya mtendaji wa kijiji cha Siwandeti wilayani humo akiwatuhumu kuendesha mambo mbalimbali yasiyofaa.  
 
Hali hiyo imesababisha wachungaji wengine zaidi ya 7 wa makanisa ya kipentekoste kutimka majumbani kwao na kukimbilia kusikojulikana ,wakihofia kukamatwa na kupewa adhabu kama hiyo ya kutembezwa uchi na jamii hiyo ya wafugaji, ambapo kwa muda mrefu jamiia hiyo na wachungaji wamekuwa hawaivani. 
 
  Mchungaji Lukumay anadai kutembezwa uchi akiwa amefungwa kengere na bati lenye maandishi shingoni, katika vijiji vya Mringaringa,Kiranyi ,Kemnyaki,Ngaramtoni ,Olevolosi , Eleray huku vijana hao wanaodaiwa kuamuriwa na wazee wa mila wakimwimbia nyimbo za kumkejeri.  
 
Udhalilishaji huo kwa viongozi wa dini umekuwa ukijirudia mara kwa mara wilayani humo , ambapo miaka kadhaa iliyopita ,wakazi wa maeneo hayo wanakumbukumbu ya mchungaji mwingine kufanyiwa vitendo vya kinyama kwa kutembezwa uchi huku kundi la vijana na watoto wakimdhihaki kwa nyimbo na maneno ya kejeri,akituhumiwa kupinga tohara.  
 
Akizungumza na wandishi wa habari alipokuwa amelazwa katika hospitali ya Seliani ,iliyopo eneo la Ngaramtoni baada ya kupata majeraha kadhaa ya kupigwa na kuishiwa nguvu,Lukumay alisema kuwa watu hao wamemdhalilisha sana baada ya kumvua nguo zote kisha kimtembeza uchi mbele ya watoto wadogo. ''kwa kweli wamenidhalilisha sana ,kwanza mimi ni mlokole nina familia na watoto wanne nampenda yesu ,nilishawaambia dini zetu haziruhusu kuingiliwa na mambo ya kimila,sasa hawaelewi wanashindwa kutengenisha masuala ya kidini na mila za asili ''alisema Lukumay huku akionyesha majeraha kadhaa yaliyotokana na kipigo. 
 
Mchungaji huyo alidai kwamba,polisi waliofika eneo hilo siku ya pili ndiyo waliomwokoa, kwani bila wao bila shaka mauti yangemfika kwa kuwa watu hao walikuwa na dhamira mbaya maana walimpiga na kumburuza kama alivyofanyiwa yesu Masiha na Wayahudi. Aidha ameiomba serikali kuingilia kati kwa kuwa mila za makabila hayo zimekuwa zikitumika vibaya ikiwemo kuwanyanyasa pale inapobainika kwamba wamejitenga na mila hizo na kuokoka. 
 
Nae katibu wa umoja wa wachungaji wa madhehebu ya kipentekoste,Joseph Kaondo amelaani kitendo hicho na kulitupia lawama jeshi la polisi kwa madai kwamba limeshindwa kudhibiti vitendo vya udhalilishaji wanavyofanyiwa watumishi wa mungu . Alisema wazee jamii ya wafugaji ndio wamekuwa wakiongoza kuwaamuru vijana kufanya msako dhidi ya wachungaji na kuwakamata , kisha kuwafanyia vitendo vya udhalilishaji bila kuchukuliwa hatua zozote.  
 
Kaimu kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha,Akili Mpwapwa alikiri kupata taarifa hizo na kudai kwamba anazifanyia kazi ikiwepo kufanya uchunguzi juu ya tukio hilo. ''ni kweli nimepata taarifa ila sisi kama polisi tunafanya uchunguzi ili kujua undani wa tukio hilo''alisema

TANZANIA NA CHINA ZATIA SAINI MIKATABA MITATU YA MIRADI YA MAENDELEO

Na Bebi Kapenya
MAELEZO, Dar es Salaam

SERIKALI ya Tanzania na ile ya China wamewekeana saini ya mikataba mitatu ya miradi mbalimbali ya maendeleo isiyo na riba yenye thamani ya Dola za Kimarekani milioni 89.7 pamoja na kubadilishana hati ya ujenzi wa kituo cha Mikutano cha Mwalimu Nyerere.

Hafla hiyo imefanyika jana Jijini Dar es Salaam, ambapo Serikali ya Tanzania imewakilishwa na Waziri wa Fedha Mustapha Mkulo na kwa upande wa China imewakilishwa na Naibu Waziri wa Biashara wa nchi hiyo Jiang Yaoping.
 
Mikataba hiyo iliyosainiwa ni katika sekta za mawasiliano pamoja na ile ya miradi mbalimbali ya maendeleo ya kijamii pia makabadhiano ya hati ujenzi wa kituo cha Mikutano cha Mwalimu Nyerere kinachotarajiwa kukamilika mwezi Mei mwakani.

Waziri Mkulo aliishukuru Serikali ya watu wa China kwa mkopo huo na kuwahakikishia kwamba Tanzania itatumia fursa hiyo kwa ajili ya kuwaletea wananchi maendeleo yaliyokusudiwa.
Waziri aliongeza kuwa Serikali ya Tanzania imeshatenga ardhi kwa ajili ya mradi wa ujenzi wa kituo cha Mwalimu Nyerere na kuongeza kuwa kinachosubiriwa kwa sasa ni fedha kwa ajili ya fidia kwa wakazi wa eneo husika.
 
Aidha Waziri Mkulo alisema, Serikali itashirikiana na Ubalozi wa China nchini ili kuhakikisha usalama wa watu wa China unakuwepo na kwamba watawashughulikia wale wote walio husika katika mauaji ya mfanyabiashara wa kichina yaliyotokea hivi karibuni.

Kuhusu madeni ya wakandarasi wa Kichina wanaofanyakazi hapa nchini Waziri Mkulo amemuahidi kiongozi huyo kulishughulikia haraka iwezekanavyo, hivyo amewataka kuendelea kuwa wavumilivu huku wakiendelea na shughuli zao.

Kwa upande wake Jiang Yaoping alisema, Serikali ya China itaendelea kuisaidia Tanzania katika miradi mbalimbali ya maendeleo na kuiomba serikali itumie misaada hiyo inavyotakiwa kwa ajili ya maendeleo ya Tanzania.

BASATA YAWATAKA WASANII KUTUMIA KISWAHILI FASAHA

Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) limewataka Wasanii kutumia Kiswahili sanifu katika kazi zao i kama hakuna sababu ya msingi ya kufanya vinginevyo hasa ya kisanii.
Akizungumza ofisini kwake wiki hii muda mfupi kabla ya Programu maalum ya kuwapa elimu Wasanii juu ya Ushairi na Utumizi wa Lugha Sanifu Katika Sanaa, Katibu Mtendaji wa BASATA, Ghonche Materego alisema kuwa, ni muhimu kwa Wasanii kutumia lugha sanifu katika kazi zao kutokana na ukweli kuwa, wanasikilizwa na watu wengi na ni kioo cha jamii.
“Wasanii wana mchango mkubwa katika kukuza Kiswahili. Wanatakiwa kutumia lugha fasaha na iliyosanifiwa ingawa hili haliwabani pale wanapotakiwa kuvaa uhusika katika kazi wanazozifanya hasa uigaji wa lafudhi na utumizi wa lugha kulingana na maeneo au mazingira” alisema Materego.
Aliongeza kuwa, kuna baadhi ya mazingira kitaaluma ndani ya Sanaa yanawaruhusu Wasanii kutumia lugha vinginevyo lakini hili ni pale tu wanapotakiwa kuvaa uhusika na si inavyofanywa na baaadhi ya Wasanii kupotosha lugha makusudi.
“Kuna suala la uhusika na ufikishaji ujumbe katika kazi za Sanaa, hili linampa fursa Msanii kuitumia lugha kulingana na haja na mazingira. Msanii akiwa katika hali hiyo kwa kweli ni katika kutekeleza majukumu yake” alisisitiza Materego.
Awali akiongea na Wadau wa Sanaa kwenye programu hiyo, Mtendaji kutoka Usanifu wa Kiswahili na Ushairi Tanzania (UKUTA), Mchamba A. Mchamba alisema kuwa, kumekuwa na upotoshaji wa lugha miongoni mwa Wasanii hali ambayo imekuwa ikivuruga Lugha hiyo.
Alitoa wito kwa Wasanii na Waandishi wa habari kuwa mabalozi wema katika kukisambaza Kiswahili sanifu kutokana na ukweli kuwa, wanaaminiwa, kusikilizwa na kusomwa sana na watu wa kada mbalimbali.
“Wasanii na Waandishi wanaaminiwa, kusikilizwa na kusomwa sana. Kila wanachoongea kinachukuliwa na jamii kama kilivyo. Ni vema wakawa mstari wa mbele kutumia lugha sanifu kwani itawapa heshima na kuipa thamani kazi yao” aliongeza.

RAIS JAKAYA KIKWETE ATUMA SALAAMU ZA RAMBIRAMBI KAGERA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia salamu za rambirambi Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Mheshimiwa Fabian Massawe kufuatia vifo vya watu 18 kutokana na ajali ya barabarani iliyotokea juzi, Jumamosi, Novemba 19, 2011, katika eneo la Lusahunga, Biharamulo, Kagera. 
 
Aidha, Rais Kikwete ametuma salamu za pole kwa watu wote 17 walioumia katika ajali hiyo ambako basi la Taqwa liligongana na lori kwenye barabara la Biharamulo-Ngara.

Katika salamu zake, Rais Kikwete amemwambia Mkuu huyo wa Mkoa, “ Nimepokea kwa masikitiko na huzuni habari za vifo vya wenzetu 18 waliopoteza maisha yao katika ajali ya basi la Taqwa. Kupitia kwako nawatumia salamu zangu za pole za dhati ya moyo ndugu, jamaa na marafiki wote waliopoteza watu katika ajali hiyo,”

Ameongeza Rais Kikwete: “Wajulisheni kuwa niko nao katika uchungu mkubwa walionao katika kipindi hiki cha maombolezo. Waambie kuwa msiba wao ni msiba wangu pia. Nawaombeeni subira na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu kwa sababu yote ni mapenzi ya Mungu. Namwomba Mwenyezi Mungu aziweka roho za marehemu pahali pema peponi. Amen.”

Ameongeza Rais Kikwete: “Kwa wenzetu walioumia katika ajali hiyo, nawatumia pole zangu nyingi. Nawatakia heri waweze kupona haraka ili warejee katika shughuli zao za kujenga taifa na za kujiletea maendeleo.”
 
IMETOLEWA NA:


KURUGENZI YA MAWASILIANO YA RAIS IKULU
NOVEMBA 21, 2011

Monday, November 21, 2011

SMZ KUSHIRIKIANA NA WANAWAKE WATAALAMU WA KILIMO NA MAZINGIRA NCHINI KUINUA HALI ZA MAISHA YA WANAWAKE

Maalim Seif akifungua mkutanao wa 15 wa mwaka wa Jumuiya ya TAWLAE.
Maalim Seif akisalimiana na viongozi na wanachama wa TAWLAE katika hafla ya ufunguzi ya mkutano wa 15 wa Jumuiya hiyo ya wanawake. 

Na Hassan Hamad, OMKR                              
 
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad amesema serikali itashirikiana kikamilifu na wanawake wataalamu wa Kilimo na Mazingira nchini katika kuhakikisha jamii inaelewa umuhimu wa kuhifadhi mazingira na kuinua hali za maisha ya wanawake.
Maalim Seif amesema hayo leo alipokuwa akifungua mkutano wa mwaka wa Chama cha Wanawake Wataalamu wa Kilimo na Mazingira (TAWLAE) huko katika ukimbi wa mikutano wa EACROTANAL mjini Zanzibar.
Maalim Seif amesema kazi zinazofanywa na jumuiya hiyo za kuwaelimisha wanawake kuhimiza matumizi ya nishati mbadala na uhifadhi wa mazingira, kuwatoa watoto kwenye ajira mbaya na kuwasomesha zinaungwa mkono na serikali na kuna haja jumuiya na mashirika mengine yaziunge mkono.
Alisema majukumu hayo ni muhimu katika kuwaletea maendeleo wanawake na kuinua maisha ya wananchi kwa ujumla kwasababu kumsaidia mwanamke ni sawa na kuisadia jamii nzima.
Alisema suala la kuhimiza matumizi ya nishati mbadala ni jambo la kupewa umuhimu wa kipekee hasa kwa vile dunia hivi sasa inashuhudia athari kubwa zilizosababishwa na mabadiliko ya tabia nchi ambayo yameathiri maisha ya watu wengi pamoja na kudidimiza uchumi wa nchi.
“Endeleeni na juhudi hizi za kueneza elimu na kuinua uelewa wa wanawake na jamii yetu, serikali zinakuungeni mkono, kwasababu tunajua mikakati hii itapelekea kuokoa mazingira yetu yasiathiriwe lakini pia zitachangia kwa kiasi kikubwa maisha ya wanawake na jamii yote kuwa bora zaidi”, alisema Maalim Seif.
Sambamba na hatua hizo zinazochukuliwa, Makamu wa Kwanza wa Rais ameishauri TAWLAE kushirikiana bega kwa bega na wadau wengine katika kupiga vita matumizi, uingizaji na usambazaji dawa za kulevya, ili kutoa mchango wao katika kuyaokoa maisha ya vijana waliojiingiza katika janga hilo, wakiwemo wasichana.
“Nashauri TAWLAE pia ijikite katika kuwaokoa vijana, hasa vijana wa kike waliozama katika matumizi ya madawa ya kulevya kwa kuwa na mipango thabiti ya kuwapatia matibabu vijana hao na kasha kuwasaidia kupata ajira”, alishauri Maalim Seif. 
Alisema kwa upande wa Zanzibar katika kupambana na matumizi ya dawa za kulevya na kuwasaidia wale waliojiingiza kwenye matumizi yake, juhudi kubwa zinaendelea kuchukuliwa, ikiwemo kujengwa nyumba za kuwapa ushauri na kuwarekebisha kitabia vijana hao (Sobber Houses), ambapo vijana wa kike na kiume wananufaika na ushauri pamoja na huduma mbali mbali.
Mapema Mwenyekiti wa TAWLAE, Christine Lyimo alisema pamoja na mafanikio ya kuwasomesha wanawake katika ngazi mbali mbali, bado TAWLAE kinakabiliwa na changamoto kadhaa, ikiwemo uwezo mdogo wa kuendeleza wanawake wengi zaidi na tatizo la baadhi ya wanachama kuchelewa kulipa ada zao.
Wakati huo huo Makamu wa kwanza wa Rais amelitaka Baraza la Manispaa Zanzibar kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi pamoja na jeshi la polisi katika kudhibiti mifugo inayozurura katika manispaa ya mji wa Zanzibar.
Amesema mifugo hiyo imekuwa ikileta kero katika mji ikiwa ni pamoja na kuchafua mazingira ya mji na kusababisha ajali, ambao ambayo yanaweza kuepukwa iwapo mifugo hiyo itadhibitiowa.
Akichangia katika mazungumzo hayo yaliyofanyika Ofisi ya Makamu wa kwanza wa Rais Migombani, kamishna wa polisi Zanzibar Mussa Ali Mussa amependekeza kuzingatiwa ushirikishwaji wa wananchi kupitia polisi jamii katika kukabiliana na tatizo hilo.
Pia kamishna Mussa amependekeza kukabiliana na chanzo cha kuzagaa kwa mifugo hiyo ambacho ni mazizi ya mifugo katika eneo la mjini, na kwamba kufanya hivyo kutarahisisha kuondoa tatizo la kuzagaa kwa mifugo katika eneo la mjini.

UZINDUZI WA MIAKA 10 YA KUZALIWA KWA CHUO KIKUU CHA TAIFA ZANZIBAR (SUZA)

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA) Prof.Idris Ahmada Rai akifafanua jambo mbele ya waandishi wa Habari ambao hawapo pichani katika uzinduzi wa Sherehe za kutimiza Miaka 10 ya Chuo hicho, kushotoni kwake ni Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Taaluma Dk. Abdallah Ismail Kanduru
Mmoja kati ya Waandishi wa Habari akiuliza Swali kwa Mkuu wa Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA) Prof.Idris Ahmada Rai ambaye hayupo pichani katika uzinduzi wa Sherehe za kutimiza Miaka 10 ya Chuo hicho kwenye hafla iliyofanyika katika Ukumbi wa Chuo hicho Vuga Mjini Zanzibar. PICHA ZOTE NA Yussuf Simai-Maelezo Zanzibar
 
Na Khadija Khamis – Habari Maelezo.
 
Makamo Mkuu wa Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar ( Suza ) Profesa Idris Ahmed Rai amesema, wakati umefika sasa Chuo hicho kuwa ni chuo chenye hadhi ya kimataifa ili kiweze kutambulika duniani kote .
 
Aliyasema hayo leo huko katika uzinduzi wa sherehe za miaka kumi ya Chuo Kikuu cha
Suza ambazo zinatarajia kufikia kilele chake siku ya tarehe 24 mwezi huu.
Katika uzinduzi huo Profesa Rai alisema kuwa, ni dhahiri kwamba kuna mengi sana zaidi ya kuyafanya katika kukiwezesha chuo hicho kuwa ni chuo kikuu na chenye hadhi ya kimataifa nchini .

Aidha alisema kuwa wakati umefika sasa Suza kutanua huduma zake za masomo na tafiti kwa jamii ya wazanzibari na ulimwengu kwa ujumla pamoja na kukuza uwiano wa karibu sana kati ya maendeleo ya nchi na ukuwaji wa elimu ya juu .
Akifahamisha kuwa ukuwaji wa elimu ya juu ni changamoto kwa taifa kwani ukuwaji huu unalenga katika kusukuma mbele maendeleo ya nchi na ukuwaji wa uchumi nchini.
 
Ameeleza kuwa mpango wa Chuo hicho unatarajia kuwa na skuli kadhaa ambazo zitatoa masomo na mafunzo tofauti ambayo ni muhimu kwa jamii yetu na mahitaji ya ulimwengu wa sayansi na teknolojia.
 
Alifahamisha kuwa ukuwaji wa chuo hicho unatarajiwa kuwa katika awamu tofauti ambapo katika awamu ya kwanza, kunatarajiwa kuanzishwa skuli ambazo zinatokana na na idara au taasisi zilizopo hivi sasa ili kuweza kutoa fursa muhimu kwa skuli na idara zake mpya kuwa na uwezo mkubwa wa kukuza programu zake.
 
Alieleza kuwa chuo kikuu cha suza kinajipanga vyema kuisaidia serikali katika kufanikisha sera yake ya kukuza utalii kwa kuweza kusomesha utalii katika chuo hicho na skuli hiyo itaundwa kuwatayarisha vijana kuwa na ujuzi wa kazi katika sekta hii ili waweze kunufaika kiajira .
 
Akifafanua azma ya chuo hicho Profesa Rai alisema kuwa, ni kukifanya chuo kua bora zaidi katika ukanda wa Afrika Mashariki na chenye kutoa elimu yenye kiwango cha hali ya juu katika vigezo vya kimataifa.