Monday, November 21, 2011

UZINDUZI WA MIAKA 10 YA KUZALIWA KWA CHUO KIKUU CHA TAIFA ZANZIBAR (SUZA)

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA) Prof.Idris Ahmada Rai akifafanua jambo mbele ya waandishi wa Habari ambao hawapo pichani katika uzinduzi wa Sherehe za kutimiza Miaka 10 ya Chuo hicho, kushotoni kwake ni Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Taaluma Dk. Abdallah Ismail Kanduru
Mmoja kati ya Waandishi wa Habari akiuliza Swali kwa Mkuu wa Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA) Prof.Idris Ahmada Rai ambaye hayupo pichani katika uzinduzi wa Sherehe za kutimiza Miaka 10 ya Chuo hicho kwenye hafla iliyofanyika katika Ukumbi wa Chuo hicho Vuga Mjini Zanzibar. PICHA ZOTE NA Yussuf Simai-Maelezo Zanzibar
 
Na Khadija Khamis – Habari Maelezo.
 
Makamo Mkuu wa Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar ( Suza ) Profesa Idris Ahmed Rai amesema, wakati umefika sasa Chuo hicho kuwa ni chuo chenye hadhi ya kimataifa ili kiweze kutambulika duniani kote .
 
Aliyasema hayo leo huko katika uzinduzi wa sherehe za miaka kumi ya Chuo Kikuu cha
Suza ambazo zinatarajia kufikia kilele chake siku ya tarehe 24 mwezi huu.
Katika uzinduzi huo Profesa Rai alisema kuwa, ni dhahiri kwamba kuna mengi sana zaidi ya kuyafanya katika kukiwezesha chuo hicho kuwa ni chuo kikuu na chenye hadhi ya kimataifa nchini .

Aidha alisema kuwa wakati umefika sasa Suza kutanua huduma zake za masomo na tafiti kwa jamii ya wazanzibari na ulimwengu kwa ujumla pamoja na kukuza uwiano wa karibu sana kati ya maendeleo ya nchi na ukuwaji wa elimu ya juu .
Akifahamisha kuwa ukuwaji wa elimu ya juu ni changamoto kwa taifa kwani ukuwaji huu unalenga katika kusukuma mbele maendeleo ya nchi na ukuwaji wa uchumi nchini.
 
Ameeleza kuwa mpango wa Chuo hicho unatarajia kuwa na skuli kadhaa ambazo zitatoa masomo na mafunzo tofauti ambayo ni muhimu kwa jamii yetu na mahitaji ya ulimwengu wa sayansi na teknolojia.
 
Alifahamisha kuwa ukuwaji wa chuo hicho unatarajiwa kuwa katika awamu tofauti ambapo katika awamu ya kwanza, kunatarajiwa kuanzishwa skuli ambazo zinatokana na na idara au taasisi zilizopo hivi sasa ili kuweza kutoa fursa muhimu kwa skuli na idara zake mpya kuwa na uwezo mkubwa wa kukuza programu zake.
 
Alieleza kuwa chuo kikuu cha suza kinajipanga vyema kuisaidia serikali katika kufanikisha sera yake ya kukuza utalii kwa kuweza kusomesha utalii katika chuo hicho na skuli hiyo itaundwa kuwatayarisha vijana kuwa na ujuzi wa kazi katika sekta hii ili waweze kunufaika kiajira .
 
Akifafanua azma ya chuo hicho Profesa Rai alisema kuwa, ni kukifanya chuo kua bora zaidi katika ukanda wa Afrika Mashariki na chenye kutoa elimu yenye kiwango cha hali ya juu katika vigezo vya kimataifa.

No comments:

Post a Comment