Tuesday, November 8, 2011

RUFANI YA MICHAEL WAMBURA

Kamati ya Nidhamu na Usuluhishi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imesema haina mamlaka (jurisdiction) ya kusikiliza shauri lililowasilishwa mbele yake na aliyekuwa mgombea uenyekiti wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Mara (FAM), Michael Richard Wambura.

Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa kamati hiyo, Kamishna Mstaafu wa Polisi Alfred Tibaigana, Wambura aliwasilisha rufani mbele yao akipinga uamuzi wa Kamati ya Uchaguzi ya TFF kumuengua kugombea uongozi katika chama hicho.

Tibaigana alisema Kamati yake ambayo ina wajumbe saba, kabla ya kusikiliza shauri hilo ilitaka kwanza kujua kama ina mamlaka (jurisdiction) hayo. Kamati ilizitaka pande zote (bothi parties)- mlalamikaji na mlalamikiwa kueleza kama ina jurisdiction au la.

Mwanasheria wa Wambura, Audax Kahendaguza aliwasilisha hoja zake za kwa nini anadhani Kamati ina mamlaka ya kusikiliza shauri hilo wakati Katibu Mkuu wa TFF, Angetile Osiah alieleza kwa nini anaamini Kamati hiyo haina mamlaka hayo.

Baada ya hapo, Kamati ilizitoa nje pande zote mbili na baadaye kufanya uamuzi. Uamuzi wa Kamati kuwa haina mamlaka hayo ulikariri Ibara ya 12(4) ya Kanuni za Uchaguzi za wanachama wa TFF inayosema: “The decisions of the TFF Elections Committee are final and conclusive and shall not be monitored by any body.”

STARS KWENDA N’DJAMENA KESHO
Timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars) inatarajia kuondoka kesho (Novemba 9 mwaka huu) saa 9 alasiri kwa ndege ya Kenya Airways kwenda N’Djamena kwa ajili ya mechi ya kwanza ya mchujo ya Kombe la Dunia dhidi ya Chad itakayochezwa Novemba 11 mwaka huu.

Msafara wa Stars wenye watu 40 ukiongozwa na Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya TFF, Eliud Mvella utawasili N’Djamena kesho hiyo hiyo saa 1.15 usiku kwa saa za huko ambapo kwa hapa nyumbani ni saa 3.15 usiku.

Wachezaji katika msafara huo watakuwa wote 21 walioko kambini, watu sita kutoka Benchi la Ufundi wakiongozwa na Kocha Jan Poulsen, wajumbe wawili wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT) na washabiki.

Stars ambayo iliagwa jana saa 1 usiku kwa kukabidhiwa bendera na Mwenyekiti wa BMT, Dioniz Malinzi itarejea nchini Novemba 13 mwaka huu saa 7.25 mchana kwa ndege ya Ethiopian Airlines na kwenda moja kwa moja kambini New Africa Hotel kujiandaa kwa mechi ya marudiano itakayochezwa Novemba 15 mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

MICHUANO YA UHAI CUP 2011
Timu 15 zinazoshiriki michuano ya mwaka huu ya Kombe la Uhai zimepangwa katika makundi matatu ambapo mechi zitachezwa katika viwanja viwili; Uwanja wa Karume na Uwanja wa Azam ulioko Chamazi, Mbande.

Mashindano hayo yanashirikisha timu zenye umri chini ya miaka 20 za klabu zote 14 za Ligi Kuu ya Vodacom wakati timu mwalikwa mwaka huu ni timu ya Taifa kwa vijana wenye umri chini ya miaka 17 (Serengeti Boys).

Mabingwa watetezi Ruvu Shooting Stars ndiyo wanaoongoza kundi A katika michuano hiyo inayodhaminiwa na Kampuni ya Said Salim Bakhresa kupitia bidhaa yake ya maji Uhai. Timu nyingine katika kundi hilo ni Oljoro JKT, Kagera Sugar, Azam na Mtibwa Sugar.

Kundi B lina timu za JKT Ruvu Stars, Polisi Dodoma, Moro United, Yanga na Villa Squad wakati kundi C ni Simba, Coastal Union, Toto Africans, African Lyon na Serengeti Boys. Mbali ya sh. milioni moja za maandalizi kwa kila timu, mdhamini pia anatoa zawadi kwa washindi watatu wa kwanza, mchezaji bora, mfungaji bora, timu yenye nidhamu na nauli za kuja Dar es Salaam na kurudi kwa timu kutoka mikoani.

Campaign Against Malaria yenyewe inatoa seti moja ya jezi kwa kila timu inayoshiriki mashindano hayo ambayo yataanza Novemba 12 na kumalizika Novemba 13 mwaka huu.

Kila siku kutakuwa na mechi tatu katika kila uwanja. Siku ya ufunguzi Toto Africans itacheza na Serengeti Boys saa 3 asubuhi Uwanja wa Karume, Ruvu Shooting Stars vs Oljoro JKT (saa 8 mchana- Karume) na Kagera Sugar vs Azam (saa 10 jioni- Karume).
Simba vs Coastal Union (saa 3 asubuhi- Chamazi), JKT Ruvu Stars vs Polisi Dodoma (saa 8 mchana- Chamazi) na Moro United vs Yanga (saa 10 jioni- Chamazi).


Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

No comments:

Post a Comment