Sunday, October 16, 2011

KENYA YAINGIA MPAKANI MWA SOMALIA

Ramani ya Kenya na Somalia

Serikali ya Kenya imethibitisha kwamba wanajeshi wake wameingia nchi jirani ya Somalia kuwasaka wanamgambo wa Al ShabaAb.

Katibu Mkuu wa wizara ya usalama nchini Kenya , Francis Kimemia, ameiambia BBC kuwa wanajeshi wao waliingia nchini Somalia siku ya Jumapili , kuwasaka wapiganaji wa kiislamu wa Al Shabaab, ambao wanatuhumiwa kuwateka nyara raia wanne wa kigeni ndani ya Kenya.
''Tayari Al Shabab wameshambulia Kenya. Wameingia ndani ya nchi , wakapiga risasi na kuchukua marafiki wa Kenya.'' Bw Kimemia amesema.
Ameongeza kuwa Kenya iko tayari kuwasaka wanamgambo hao popote walikojificha ndani ya Somalia.
Wiki iliyopita, wapiganaji wa Al Shabaab waliwateka nyara maafisa wawili wa shirika la kutoa misaada, la madaktari wasiokuwa na mipaka (MSF) , katia kambi ya wakimbizi ya Dadaab, kaskazini mwa Kenya.
Wageni wengine wawili pia walitekwa nyara hapo kabla katika mji wa Lamu, mwambao wa Kenya. Wageni hao ni pamoja na watalii wawili, raia wa Uingereza na Ufaransa.
Mwandishi wa BBC alioko kaskazini mashariki mwa Kenya anasema wanajeshi wa Kenya waliingia Somalia Jumapili asubuhi.
Na habari alizopata kutoka Somalia zinaarifu kuwa wanajeshi wa Kenya wakiwa na vifaru wameingia hadi kilomita 90 ndani ya Somalia.
Serikali ya mpito ya Somalia imekanusha kuwa wanajeshi wa Kenya wako ndani ya nchi yao. Balozi wa Somalia nchini Kenya, Mohammed Ali Noor , amesema kuwa ripoti walizonazo ni kwamba Kenya imeimarisha ulinzi kwenye mpaka na nchi ya Somalia na kwamba vikosi vyake havijaingia nchini Somalia.
'' Wanajeshi wa Kenya wameimarisha ulinzi kwenye mpaka na wako upande wa Kenya. Hakuna mwanajeshi yeyote ambaye yuko kwenye ardhi ya Somalia'', Balozi Ali Noor amesema.

No comments:

Post a Comment