Thursday, July 26, 2012

MELI TATU ZAFUTIWA HATI YA KUFANYA KAZI ZANZIBAR.


Kaimu Mkurugenzi Mamlaka ya Usafiri wa Baharini Zanzibar Abdullah Husein Kombo

Mamlaka ya Usafiri wa Baharini Zanzibar imezifutia rasmi hati ya kufanya kazi Meli ya Mv.Kalama, Mv.Seagul na Mv.Sepideh kutokana na meli hizo kutokukidhi hali ya usalama wa abiria katika meli hizo.

Aidha meli hizo zimepewa muda wa mwezi mmoja kuanzia leo kuhakikisha zimeondoka katika maeneo ya Zanzibar kabla ya hatua zaidi kuchukuliwa dhidi ya wamiliki wa Meli hizo.

Kauli hiyo imetolewa na Kaimu Mkurugenzi Mamlaka ya Usafiri wa Baharini Zanzibar Abdullah Husein Kombo wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari Afisini kwake kuhusu hali ya usafiri wa baharini na usalama Zanzibar.
Amesema Mamlaka hiyo imefanya tathmini na uhakiki wa kutosha na kujiridhisha kuwa Meli hizo hazifai kufanya kazi katika maeneo ya Zanzibar jambo ambalo limepelekea kuchukua hatua za kufuta hati za kufanyia kazi meli hizo.

Amefahamisha kuwa sababu kuu zilizopelekea Mamlaka kufanya maamuzi hayo ni pamoja na uchakavu,umri wa meli hizo kuwa mrefu na kupata matatizo mara kwa mara katika safari zao.

Kombo amefahamisha kuwa Sheria ya Mamlaka ya Usafiri na Bandari Zanzibar ya mwaka 2006 kifungu cha 17.1 inampa mamlaka Msajili wa Meli kuifuta meli yoyote ambayo itakuwa haikidhi usalama wa abiria.

Kufuatia sheria hiyo Kombo amesema watawataka wamiliki wa Meli hizo kuzirudisha hati za kufanyia kazi meli hizo ili waende kutafuta sehemu nyengine za usajili kinyume na maeneo ya Zanzibar.

Akizungumzia Meli ya Mv.Serengeti Kombo amesema wamelazimika kuiagiza meli hiyo kupunguza idadi ya abiria kutoka watu 800 hadi 350 na tani za mizigo kutoka 100 hadi 50  hadi pale ambapo watajiridhisha kutokana na hali ya meli hiyo ilivyo.

Aidha amegusia kuwa Kampuni ya Bakhresa italeta Meli kubwa ya abiria itakayofanya kazi zake Zanzibar ambapo pia Serikali ya Mapinduzi nayo iko mbioni kuhakikisha wanaleta meli inayokidhi mahitaji ya wananchi wa Zanzibar.


Na Faki Mjaka-Maelezo Zanzibar
26/07/2012

SERIKALI YA MAPINDUZI YA ZANZIBAR NA VIKOSI VYA ULINZI PAMOJA NA TAASISI ZA KIRAIA WAPONGEZWA

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akizungumza na Mkuu wa Mabalozi wa Nchi za Nje waliopo Tanzania Bwana Juma Alfan Mipango hapo Ofisini kwake Baraza la wawakilishi Mbweni.
Pembani yao ni Balozi wa Umoja wa Falme za Kiarabu { UAE } Bw.Mallallah  Mubarak Alameri.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi  akizungumza na Meneja Uhusiano wa Mfuko wa Pencheni wa PPF Bibi Lulu Mengele aliyefika Zanzibar kutoa mkono wa pole kwa niaba ya Uongozi wa Mfuko huo kufuatia ajali ya meli ya hivi karibuni karibu na Kisiwa cha chumbe Zanzibar.

Meneja Uhusiano wa Mfuko wa Pencheni { PPF } Bibi Lulu Mengele akiwasilisha salamu za rambi rambi kwa Makamu wa PILI WA Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi kufuatia ajali ya Meli ya M.V.Skagit iliyotokea wiki iliyopita.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akibadilishana mawazo na Bishop Michael wa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Zanzibar mara baada ya kuwasilisha salamu zao za rambi rambi hapo ukumbi wa Baraza la wawakilishi Mbweni.
Pembeni ni Katibu Mkuu wa Dayosisi hiyo Bwana Nuhu Sallanya.
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa ushirikiano na Vikosi vya Ulinzi, pamoja na Taasisi za Kiraia imepongezwa kwa hatua  iliyochukuwa  katika kukabiliana na Maafa yaliyotokea ya kuzama kwa Meli ya M.V. Skagit wiki iliyopita.
Pongezi hizo zimetolewa na Uongozi wa Taasisi tofauti zinazoendelea kutoa mkono wa pole  hapa Zanzibar kufuatia vifo vya watu kadhaa waliokuwemo ndani ya Meli hiyo iliyopata ajali karibu na Kisiwa cha Chumbe.
Afisa Uhusiano wa Mfuko wa Pencheni { PPF } Bibi Lulu Mengele Bishop  Michael wa Kanisa la Anglicana Dayosisi ya Zanzibar pamoja na Balozi wa Umoja wa Falme za Kiarabu { UAE } Bwana Mallallah Mubarak Alameri wakitoa mkono huo wa pole kwa Balozi Seif walisema hatua hiyo imesaidia kuokoa maisha ya wananchi kadhaa.
Walisema walio wengi wameshuhudia jitihada hizo za uokozi zilizoleta matumaini ndani ya nyoyo za Jamii.

Hata hivyo wawakilishi hao wa taaasisi tofauti walisema licha ya juhudi hizo za Serikali lakini bado ipo haja ya msingi ya kufuatwa kwa sheria na Taratibu sa usafiri wa Baharini.
Walisema utaratibu huo mbali ya kupunguza zinazoweza kuepukwa lakini pia utasaidia kuondosha mwanya kwa Wafanyabiashara na Wawekezaji wakorofi wanaoendesha biashara hiyo ya vyombo vya usafiri wa Baharini.
“ Kitu cha msingi ni kufuatwa kwa sheria na taratibu za usafiri nah ii itaondosha uzembe na ujanja unaotumiwa na wafanyabiashara wakorofi”. Alisisitiza Balozi wa UAE Bwana Mallallah.

Naye kwa upande wake Bishop Michael wa Kanisa la Anglikana la Mkunazini Dayosisi ya Zanzibar amesema hatua za serikali za kurejesha hali ya amani kufuatia fujo za  baadhi ya Vijana zilizofanywa hivi karibuni imeleta faraja kwa waumini wa kanila lao.
Bishop Michael alisema Uongozi wa Kanisa hilo utaendelea kuwaelimisha Waumini wao kulinda na kuheshimu amani ya Taifa ambayo inahitajiwa na kila mwana Jamii.

Akitoa shukrani zake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema Viongozi wa Serikali wanaendelea kupata matumaini kuona Taasisi na mshirika mbali mbali ndani na nje ya Nchi yanaunga mkono juhudi za Serikali.
Balozi Seif alisema Serikali kwa upande wake itaendelea kuchukuwa hatua madhubuti ili kuzuia majanga yanayoweza kuwepukwa ambayo yamo ndani ya uwezo wa mwanaadamu.
“ Tumeanza kuchukuwa hatua za kukabiliana na hali hii kwa kuwaomba washirika wetu ndani na nje ya Nchi kutusaidia katika sekta hii Likiwemo hili zito la upatikanaji wa meli kubwa ya usafirishaji wa wabiria na mizigo”. Alifafanua Balozi Seif.

 Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
26/7/2012.
 

Friday, December 2, 2011

KWAHERI MR. EBBO

Msanii Mr Ebbo afariki dunia leo akiwa mkoani Arusha ambapo inasemekana alikuwa akiumwa katika hospitali ya Mount meru.Mr Ebbo alishawahi kufanya vizuri na wimbo wake wa "mi mmasai"

Thursday, November 24, 2011

STAR TIMES YAPATA KIBALI CHA KURUSHA MATANGAZO YA TELEVISHENI ZANZIBAR

Makamu wa kwanza wa Rais wa Zanzibar maalim Seif Sharif Hamad akipokea zawadi ya kompyuta ya dijital kutoka kwa Naibu Waziri wa mawasiliano ya Habari wa China Li Wei katika shamrashamra za uzinduzi wa kampuni ya Star Times ya China ambayo imepewa leseni kuendesha shughuli zake za matangazo ya Televisheni kwa dijital hapa Zanzibar.
Maalim Seif akizungumza katika uzinduzi wa kampuni ya Star Times ya China huko Hoteli ya Zanzibar Beach Resort Zanzibar.
Maalim Seif akipongezana na Naibu Waziri wa habari wa China baada ya uzinduzi wa kampuni ya Star Times. Kulia ni Waziri wa habari, utamaduni, Utalii na Michezo Zanzibar Abdillahi Jihadi Hassan. (Picha, Salmin Said- OMKR).

Hassan Hamad (OMKR)

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imetoa kibali rasmi cha kuiruhusu kampuni ya Star Times ya China kuendesha shughuli zake za matangazo ya televisheni kwa kutumia mfumo wa kisasa wa dijital.

Akizindua mpango huo huko hoteli ya Zanzibar Beach Resort Zanzibar, Makamu wa kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad amesema kuwepo kwa kampuni hiyo kutakuza ushirikiano wa muda mrefu kati ya China na Zanzibar.

Ameitaka kampuni hiyo kuendesha shughuli zake kwa kuzingatia maadili ya wazanzibari sambamba na kufuata sheria za nchi, na kwamba serikali itafanya kazi bega kwa began a kampuni hiyo katika kuhakikisha kuwa inaendesha shughuli zake bila usumbufu.

Amesema licha ya kampuni hiyo kuwepo kibiashara, lakini itasaidia kutoa ujuzi kwa wazalendo, pamoja na kutoa nafasi za ajira kwa vijana wa Zanzibar ambao wengi wao wanasomea sekta ya habari bila ya uhakika wa ajira zao.

Amefahamisha kuwa China ni rafiki wa kweli wa Zanzibar na kwamba serikali inathamini sana mchango wa nchi hiyo katika nyanja mbali mbali za maendeleo na bado inakaribisha makampuni zaidi ya kichina kuja kuwekeza miradi yao.

Ameiomba kampuni hiyo pia kuzingatia hali ya uchumi wa Zanzibar, ili waweke viwango vya malipo ambavyo wazanzibari wengi wataweza kuvimudu na kuitumia televisheni hiyo kwa kupata taaluma na burudani zitakazotolewa.

Kampuni ya Star Times ya China ni kampuni ya mwanzo ya kigeni kuruhusiwa kuendesha shughuli hizo za habari hapa nchini, lakini tayari inaendesha shughuli zake kwa mikoa saba ya Tanzania Bara na ina wateja wapatao 140,000.

Mwenyekiti wa kampuni hiyo Pang Xin Xing amesema leseni hiyo ni hatua muhimu katika kufikia matarajio yao ya kukuza ushirikiano na kuelimisha jamii juu ya mambo mbali mbali ya maendeleo, tamaduni na kukuza biashara.

Kabla ya uzinduzi huo Makamu wa kwanza wa Rais alikutana na Naibu Waziri wa mawasiliano ya habari wa China Bw. Li Wei ambaye ameelezea matumaini yake ya kuendelea kwa uhusiano wa muda mrefu baina ya pande hizo mbili.

Bw. Li amesema ushirikiano uliopo haulengi baina ya serikali kwa serikali pekee bali unatapakaa katika nyanja mbali mbali zikiwemo vyombo vya habari wakati ambapo tayari matangazo ya Televisheni ya taifa ya China ya CCTV News na yale ya Radio China Kimataifa CRI yanapokelewa vizuri na wananchi wa Zanzibar.

KUKIMBILIA SEKTA BINAFSI KWA WATAALAM NI ATHARI KUBWA KWA SEKTA YA UMMA


Na Nafisa Madai Maelezo -Zanzibar

WAZIRI wa Sheria na Katiba, Abubakari Khamis Bakary, amesema kasi ya wataalamu wanaokimbilia sekta binafsi, imekuwa na athari kubwa katika kuleta ufanisi na mageuzi katika sekta ya umma.

Hayo aliyaeleza wakati akifungua warsha ya maendeleo ya rasilimali watu kwa wataalamu wa Shirikisho la Mawasiliano la Kusini mwa Afrika (SATA), kwaniaba ya Waziri wa Miundombinu na Mawasiliano na Uchukuzi huko katika ukumbi wa hoteli ya Zanzibar Ocean View mjini zanzibar.

Waziri huyo alisema baadhi ya watu wanaona utaratibu huo ni njia muafaka kwa kuwa watalaamu wanapata fursa ya kuchangia ujuzi wao katika sekta zote za uchumi.

Waziri Bakary, alisema mtazamo huo unahitaji kuungwa mkono na wote kwa kuwa sekta binafsi na umma zina nafasi sawa katika ujenzi wa uchumi katika mataifa hayo.

Alisema Zanzibar kama sehemu ya dunia imekuwa ikipoteza wataalamu wake wengi, wanaokwenda kufanya kazi katika nchi nyengine, wakitafuta uzoefu na maslahi zaidi.

Waziri Bakary alisema hakuna nchi yoyote duniani inayoweza kuwadhibiti au kuwafungia wataalamu wake wasitoke ndani ya nchi zao, lakini kama nchi wanachohitaji kukifanya ni kutengeneza fursa za ajira pamoja na kulipa mishahara mizuri kwa ajili ya wataalamu wa ndani.

Naye Mtendaji Mkuu wa Posta Tanzania, Said Amir.Said alisema, teknolojia ya mawasiliano imekuwa ikibadilika haraka sana hivyo lazima wataalamu wa mawasiliano nao kubadilika kwa ajili ya rasilimali watu.

Aidha alieleza mkutano huo umekuwa fursa nzuri kwa Zanzibar kutambulika wakati huu mkonga wa mawasiliano ukitarajia kuchukua nafasi katika visiwani vya zanzibar

Jumla ya wataalamu wa nchi 10 za Shirikisho la SATA walishiriki katika mkutano huo zikiwemo Msumbiji, Botswana, Namibia, Zimbabwe, Afrika Kusini, Malawi, Zambia na Tanzania.

Mkutano huo wa siku tatu ambao unatarajiwa kufungwa leo hii wataalamu hao wataweza kupata fursa ya kutembelea maeneo kadhaa ya mji wa zanzibar ikiwemo kizimbani ambako watakagua mashamba ya spice, mji mkongwe.

MASHIRIKIANO ZAIDI YANAHITAJIKA KUTOKOMEZA MIFUKO YA PLASTIKI: MAALIM SEIF

Kamishna wa polisi Zanzibar Mussa Ali Mussa akitoa rai mbele ya makamu wa kwanza wa Rais maalim Seif Sharif hamad katika kufanikisha operesheni za kutokomeza mifuko ya Plastiki Zanzibar.
Maalim Seif akizungumza na kikosi kazi cha kupambana na mifuko ya plastiki ukumbi wa mikutano katika OMKR Migombani.(Picha, Salmin Said- OMKR)

Hassan Hamad (OMKR).

Makamu wa kwanza wa Rais wa Zanzibar maalim Seif Sharif Hamad amesema mashirikiano zaidi yanahitajika katika kutokomeza matumizi ya mifuko ya plastiki Visiwa Zanzibar.

Sambamba na hilo Maalim Seif amesisitiza elimu zaidi itolewe kwa wananchi ili kutambua athari za matumizi ya mifuko hiyo ambayo imekuwa ikilalamikiwa kuwa chanzo kikuu cha uchafu katika manispaa ya mji wa Zanzibar.

Maalim Seif alikuwa akizungumza na kikosi kazi cha kupambana na matumizi ya mifuko ya plastiki huo Ofisni kwake migombani, kinachowashirikisha watendaji 10 wakiwemo kutoka jeshi la polisi, Wizara ya Biashara na idara ya Mazingira.

Amesema licha ya mafanikio yaliyopatikana tangu kikosi kicho kizinduliwe rasmi na kuanza kazi miezi michache iliyopita, bado juhudi zaidi zinafaa zichukuliwe kwa kulishirikisha kikamilifu jeshi la polisi katika operesheni zinazofanywa za kuisaka mifuko ya plastiki na kuifanya Idara ya mazingira kuwa mratibu mwezeshaji wa operesheni hizo.

Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa kwanza wa Rais Mhe. Fatma Abdulhabib Fereji ambaye alishiriki katika mazungumzo hayo amesema ni vyema kikosi hicho kikaangaliwa upya ili kutoa fursa kwa jeshi la polisi kuongoza operesheni hizo.

Mhe. Fereji pia ameahidi kusimamia kanuni za sheria ya kutoa adhabu kwa watu watakaopatikana na mifuko hiyo ambayo kwa ujumla inakaribia kukamilika na kuchapishwa katika gazeti rasmi la serikali ili iweze kufanya kazi.

Kikao hicho pia kilihudhuriwa na kamishna wa polisi Zanzibar Mussa Ali Mussa amesema bado kuna fursa nzuri ya kufanikiwa kwa operesheni hizo iwapo zitawahusisha viongozi wa shehia na kutekeleza mpango wa polisi jamii katika visiwa vya Unguja na Pemba.

Watendaji wa kikosi hicho kwa upande wao wameelezea changamoto zinazowakabili ikiwa ni pamoja na ukosefu wa vitendea kazi hasa usafiri, pamoja na kutokuwepo sheria madhubuti ya kuwahukumu wanaokamatwa na mifuko hiyo.

Wamesema hali hiyo inawafanya wananchi kutokuwa na hofu kwa vile hakuna sheria inayowabana, na hivyo kulifanya zoezi hilo kuwa gumu.

Kikosi kazi hicho kimeiomba serikali kusimamia utekelezaji wa maagizo yake katika mamlaka zinazohusika, wakidai kuwa mifuko mingi kati ya inayoingia nchini inapitia katika bandari kuu ya Zanzibar huku watendaji wa mamlaka hiyo wakifumbia macho agizo hilo.